Katika Kikao cha Baraza Kuu la Chadema kinachoendelea kwa sasa, Mbowe anatazamia kuwakilisha jina hilo mbele ya wajumbe wa baraza hilo ili kujaza nafasi iliyoachwa na Dk. Willibrod Slaa, aliyejienguwa ukatibu mkuu wa chama hicho.Dk. Slaa aliondoka Chadema muda mfupi baada ya chama hicho kumpitisha Edward Lowassa aliyetokea CCM kuwa mgombea urais wa chama hicho na kuungwa mkono na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Licha ya kwamba haijajulikana na ni nani hasa anayeenda kutwaa nafasi hiyo lakini wanaotajwa ni pamoja na Salum Ally Mwalimu, Frederick Sumaye, Benson Kigaila, John Mnyika, Dk. Marcus Albanie na Prof. Mwesiga Baregu.
Taarifa kutoka Mwanza zinaeleza kwamba, kama hakutakuwa na vuta nikuvute chama hicho kinaweza kufikia muafaka bila kufikia hatua ya upigaji kura.
Taarifa hizo zinaeleza kwamba, Katibu Mkuu huyo mpya atakuwa na kazi ya kuhakikisha kuwa chama hicho kwa kushirikiana na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kushika dola kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2020.
Kishindo cha upinzani nchini kinatarajiwa kuanza upya hivi karibuni baada ya chama hicho kukamilisha mkakati wa kujipanga upya.
Kwa miezi minne mfululizo baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, 2015, Ukawa vimekuwa kimya kiasi cha kuzua shaka kwa wananchi, hata Rais John Magufuli kuanza kutamba kwamba, ataua upinzani.
Mtandao huu una taarifa kwamba Chadema, chama kiongozi katika Ukawa, kinajipanga kuamka kwa nguvu mpya nchi nzima kuanzia katika sakala la umeya wa Jiji la Dar es Salaam.
Kadiri serikali itakavyojitahidi kuhujumu Ukawa, taarifa zinaeleza, ndivyo Chadema itakavyotumia fursa hiyo kujijenga upya kisiasa.
Umuhimu wa Jiji la Dar es Salaam katika siasa za Tanzania na ubabe unaotumiwa na serikali kuzuia uchaguzi wa meya wa jiji ili kuzuia wapinzani kuongoza Jiji la Dar es Salaam ni sehemu ya fursa ambazo, zikitumiwa vema zitaamsha siasa za upinzani na kuua CCM Dar es Salaam.
0 comments:
Post a Comment