Home » » LIPUMBA ATANGAZA NIA

LIPUMBA ATANGAZA NIA


Prof. Ibrahim Lipumba akikabidhiwa fomu na Katibu wa CUF wilaya ya Kinondoni, Mohamed Mkandu,
Prof. Ibrahim Lipumba akikabidhiwa fomu na Katibu wa CUF wilaya ya Kinondoni, Mohamed Mkandu,

MWENYEKITI wa Chama cha Wananchi (CUF) Profesa Ibrahim Lipumba, leo amechukua fomu na kutangaza nia ya kugombea urais kupitia chama hicho huku akiahidi kuunda serikali ya umoja wa kitaifa kukabiliana na ufisadi.  
Mbali na kuunda serikali ya umoja wa kitaifa, amesema ataweka lengo binafsi la kuongoza nchi kwa haki ili aweze kuwa rais wa kwanza wa Tanzania kushinda tuzo ya uongozi uliotukuka na wenye mafanikio kwa marais wa Afrika, ‘Tuzo ya Mo Ibrahim’.
Hii inatajwa kuwa tuzo kubwa zaidi duniani kwani mshindi hupatiwa fedha ikilinganishwa na tuzo nyingine duniani. Tuzo hii ilianzishwa mwaka 2007.
Prof. Lipumba ambaye pia ni Mwenyekiti mweza wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) amekabidhiwa fomu hiyo na Mohamed Mkandu, Katibu wa CUF wilaya ya Kinondoni, baada ya kulipia gharama ya Sh. 500, 000.
Prof. Lipumba ametangaza nia ya kuutaka urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mbele ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar  (SMZ) ambaye pia ni Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharrif Hamad, viongozi wa chama na maelfu ya wananchama wa chama hicho.
Tofauti na ilivyotarajiwa ukumbi huo ulifurika wafuasi wa chama hicho hali iliyopelekea wengine kubaki nje ya ukumbi wakisubiri angalau kumuona kiongozi wao.
Lipumba amesema “nimechukua fomu kupitia chama changu kama ambavyo utaratibu unataka. Kisha kama UKAWA wataniona nafaa watanipendekeza kugombea urais.”
Amesema iwapo UKAWA itampitisha kuwania urais, serikali watakayoiunda itahakikisha maoni ya wananchi, yaliyonyofolewa na Bunge Maalum la Katiba lililoongozwa na CCM yanarejeshwa hasa katika vipengele vya mfumo wa muungano, uadilifu na uwajibikaji.
“Tatizo la ufisadi linachangiwa na viongozi kupewa zawadi. Rasimu ya wananchi ikiweka kifungu kinachowataka viongozi kutoa taarifa na kuzikabidhi zawadi hizo serikalini, lakini mafisadi wamekiondoa kifungu hichi.
Aidha, amesema Bunge hilo liliondoa kipengele cha viongozi watanzania kutoruhusiwa kuwa na akaunti za benki nje ya nchi ili kuepuka uibaji wa fedha zinazofichwa nje ya nchi. Hali ambayo inachochea vitendo vya kifisadi kuendelea kushamili.
Amesema tatizo ni matumizi mabaya ya fedha za umma na ufisadi uliokithiri. Katika ripoti Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za  Serikali, kuhusu akaunti ya Tegeta Escrow ameonesha makosa ya jinai ya kughushi nyaraka na kukwepa kodi.
“Makosa yapo wazi, lakini mpaka hivi sasa waliohusika hawajafikishwa mahakamani. Na wengine waliochota fedha hizo wanazitumia kutafuta wadhamini ili wagombee urais kwa tiketi ya CCM,” amefafanua Prof. Lipumba.
“Kama nitapewa ridhaa na Ukawa, sina mswalia Mtume na mafisadi. Nitahakikisha uwazi, uwajibikaji na uadilifu ziwe ni tunu za taifa,” ameeleza Prof. Lipumba.
Ameeleza pia atahakikisha matatizo ya ukosefu wa lishe kwa watoto yanakoma ikiwa ni sehemu ya kujenga taifa imara, kuhakikisha haki ya uzazi salama, ujenzi wa miundombinu, uwezeshwaji wa watoto wa kike ikiwemo kukomesha mimba za utotoni, kumaliza magojwa ya malaria na kifua kikuu na kuanzisha hifadhi ya wazee.
“Katika kila watoto 100 watoto 42 wana udumavu unaosababishwa na kutopata lishe bora. Ukimnyima mama na mtoto lishe bora nikuwanyima maendeleo.
“Lazima akina mama wapate fursa ya kujifungua salama. Tutahakikisha tunawapa fursa watoto wa kike ili kujiendeleza kielimu,” ameeleza Prof. Lipumba.
Prof. Lipumba amesema, “Hivi sasa tayari kuna matatizo ya panya road ni kwa sababu ya kukosa ajira na kukosa matumaini . Ni lazima tujenge mazingira ya kuwapatia watanzania ajira za kutosha.”
Aidha, Hamad amesema Tanzania ipo tayari kwa mageuzi, watanzania wamechoka na ukandamizaji. Na ili kuyapata mabadiliko hayo ni lazima wafanye maamuzi kwa kutumiaUKAWA.
Akitaja sifa za Rais, Hamad amesema, “hatakiwi kuwa mbinafsi, ayaweke matatizo ya wananchi rohoni na moyoni, mwenye upeo mkubwa wa kuona mambo, kujenga uchumi imara na madhubuti, mwenye mawazo mapya, ahakikishe rasilimali zote zinawanufaisha watanzania wote.”
Prof. Lipumba aliyewahi kuwa mshauri wa masuala ya uchumi wa Rais wa awamu ya pili, Ali Hassan Mwinyi alizaliwa 6 June 1952, Ilolangulu, Tabora. Ni Mwanasiasa na Mchumi wa kimataifa. Ameoa mke mmoja. Mwaka 1959 – 1966 Alisoma elimu ya msingi.
Mwaka 1967 – 1970 alisoma Shule ya Sekondari ya wavulana ya Tabora na kuhitimu elimu ya kidato cha sita mwaka 1972 katika Shule ya Sekondari ya Pugu ambapo mwaka 1973 alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam  ambapo alisomea uchumi ngazi ya Shahada.
Mwaka 1978 alitunukiwa shahada ya pili ya uchumi baada ya masomo ya uchumi  chuo Kikuu cha Dar es Salaam na mwaka 1978 alijiunga Chuo Kikuu cha Marekani cha Stanford ambapo alisoma uchumi na kutunukiwa PHD.
Toa maoni yako kwa habari hii kwa kuweka email yako hapa,na endelea kutufatilia zaidi Ukurasa wa habari

0 comments:

 
Supported by AMAGA Media services : | |
Copyright © 2015. UKURASA WA HABARI - All Rights Reserved
Templete Designed by Abdallah Magana
Proudly powered by Blogger