WABUNGE
wameitaka Serikali kuharakisha mazungumzo yake kuhusu tatizo lililopo la
mgomo wa wafanyabiashara nchi nzima, ili suala hilo lipatiwe ufumbuzi
mapema.
Hayo
yalibainishwa bungeni hapo na Naibu Spika Job Ndugai, wakati wakati
akijibu miongozo mbalimbali iliyoombwa na wabunge kuhusu suala hilo
ambao wengi wao walitaka mijadala ya Bunge hilo iahirishwe ili suala
hilo lijadiliwe kama dharura.
Hata
hivyo, Ndugai alisema kutokana na hali halisi iliyopo sasa ni muhimu
mazungumzo hayo yakaendeshwa kwa haraka ili kufikia mwafaka na kupata
ufumbuzi wa mgogoro uliopo.
Jana
takribani wabunge watano, kabla ya mijadala ya miswada haijaanza
kujadiliwa, waliomba mwongozo wa Spika wakitaka Serikali itoe tamko juu
ya mgomo unaoendelea nchini kwa kuwa pamoja na shughuli za kiuchumi
kusimama wananchi wanaatabika na kukosa huduma.
Mbunge wa
Njombe Kaskazini, Deo Sanga (CCM), aliitaka Serikali kutoa tamko kuhusu
tatizo lililopo kwa kuwa linazidi kuongezeka hasa baada ya
wafanyabiashara kuongezewa kodi kwa asilimia 100, huku mwenyekiti wao,
Johnson Minja, bado akiwa mahabusu.
Naye
Mbunge wa Tabora Mjini, Ismail Aden Rage (CCM) alisema serikali haipaswi
kulipuuzia suala hilo kwa kuwa kasi ya kusambaa kwa mgomo wa
wafanyabiashara imekuwa ikiongezeka kwa kasi nchi nzima.
Kwa
upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uchumi, Viwanda
na Biashara, Luhaga Mpina, alisema maelezo aliyotolewa na Waziri wa
Fedha yanatofautiana na makubaliano yaliyofikiwa kati ya Waziri Mkuu,
Mizengo Pinda na wafanyabiashara walipokutana mwishoni mwa wiki.
Alisema
baada ya kamati yake kubaini kuwepo kwa mgogoro baina ya Serikali na
wafanyabiashara, hususani eneo la kodi na kushikiliwa kwa mwenyekiti wao
Minja na mashine za EFDs, iliandaa mpango wa kukutanisha pande zote
mbili kwa ajili ya kupata mwafaka.CHANZO: HABARI LEO (MURO)
0 comments:
Post a Comment