Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum.
SERIKALI
imewasilisha mwelekeo wa bajeti kwa Kamati ya Bunge, ambayo inalenga
zaidi kupeleka umeme na huduma za maji vijijini, kumalizia miradi ambayo
haijakamilika na kutenga fedha kwa ajili ya uchaguzi mkuu ujao.
Waziri wa
Fedha, Saada Mkuya Salum alisema wanaandaa bajeti ambayo itasaidia
kumaliza mambo yote waliyoahidi, ambayo yameainishwa kwenye Ilani ya
Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambayo serikali iliahidi wakati wa kampeni za
uchaguzi mkuu uliopita.
"Bajeti
ya mwaka 2015/16 ni ya kipekee. Ni mwaka wa uchaguzi, ni mwaka ambao
serikali ya Awamu ya Nne inamaliza muda wake na serikali mpya kuingia
madarakani. "Ni mwaka ambao Mkukuta na Mpango wa Kwanza wa Maendeleo ya
Milenia ya miaka mitano inafikia tamati, Malengo ya Milenia ya mwaka
2015 yanafikia ukomo na pia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama
Cha Mapinduzi ya mwaka 2010 unakamilika," alisema.
Vipaumbele vya bajeti
Akiwasilisha
mwelekeo wa bajeti hiyo kwa wabunge jijini Dar es Salaam jana, Mkuya
alisema bajeti ya mwaka huu imejikita zaidi kutathmini na kuangalia
changamoto kwenye sekta ya maji, nishati, rasilimaliwatu na kumalizia
miradi ambayo haijakamilika.
"Vipaumbele
kwenye bajeti hii vimejikita zaidi kwenye kuandaa awamu ya pili ya
Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano utakaoanza Juni mwaka 2016, na mkazo
zaidi ni kwenye miradi ya umeme vijijini, maji vijijini, kuimarisha
rasilimaliwatu na kugharamia uchaguzi mkuu," alisema Mkuya.
Akifafanua,
alisema katika mwelekeo huo wa Bajeti mpya ya mwaka 2015/16, jumla ya
Sh takribani trilioni 23 zinatarajiwa kukusanywa na kutumika katika
matumizi ya maendeleo na ya kawaida.
Alisema
katika matumizi ya maendeleo,vipaumbele vitano ambavyo vimetajwa hapo
juu (maji, umeme, rasilimaliwatu, kumalizia miradi viporo na kugharamia
uchaguzi mkuu). Jumla ya fedha zilizotengwa ni Sh trilioni 5.8.
Mchanganuo
wake ni kwamba fedha za ndani ni Sh trilioni 4.3 na fedha za nje ni Sh
trilioni 1.4 ambazo kwa ujumla zitatumika kwenye utekelezaji wa
vipaumbele vilivyoainishwa na kumalizia miradi ambayo haikukamilika
kwenye bajeti iliyopita.
Katika
sekta ya nishati, kipaumbele kimewekwa katika kuendeleza miradi ya umeme
vijijini, ambapo hadi sasa wateja 2,602 wa vijijini kwenye mikoa ya
Simiyu, Singida, Kagera,Tanga, Ruvuma na Iringa, wameunganishiwa umeme.
Aidha,
katika sekta ya maji vijijini, tathmini ya bajeti iliyopita, inaonesha
kuwa jumla ya miradi ya maji vijijini, ilikuwa 123 iliyojengwa na
kukamilika na idadi hiyo imewanufaisha wananchi 463,750.
Katika
bajeti hii, mkazo umewekwa katika kukamilisha miradi ya maji vijijini
ambayo haijakamilika, ikiwemo miradi ya ujenzi wa mabwawa ya Kawa mkoani
Rukwa, Bwawa la Sasajila lililopo Dodoma na bwawa la Mwanjoro lililopo
Shinyanga pamoja na miradi mingine kwenye maeneo mengine vijijini.
Akizungumzia
suala la Uchaguzi Mkuu, unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu, ambalo
ni moja ya vipaumbele katika bajeti hiyo mpya, Mkuya alisema bajeti
imejikita katika kugharamia uchaguzi huo ili ufanyike na kupata serikali
mpya itakayoendelea kutekeleza bajeti hii.
Mwelekeo wa bajeti
Akizungumzia
mwelekeo wa bajeti, Mkuya alisema Serikali imepanga kutumia Sh trilioni
22.48 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo katika bajeti ya
mwaka 2015/16 huku utegemezi wa fedha za kigeni ukipungua kutoka
asilimia 14.8 ya mwaka wa fedha uliopita hadi asilimia 8.4 kwa mwaka
ujao wa fedha.
Bajeti ya mwaka 2014/15 ilikuwa ni Sh trilioni 19.9, hivyo mwelekeo wa bajeti hiyo inakuwa na ongezeko kwa takribani asilimi 16.
Alisema
katika fedha hizo, sh trilioni 16.71 zimetengwa kwa ajili ya matumizi ya
kawaida, ikijumuisha Sh trilioni 6.61 kwa ajili ya mishahara ya
watumishi wa Serikali na taasisi, Sh trilioni 3.41 kwa ajili ya matumizi
mengineyo ya Wizara huku mikoa ikiwa ni Sh bilioni 83.55 na Mamlaka za
Serikali za Mitaa ni Sh bilioni 208.75 wakati Sh trilioni 2.60
zikitengwa kwa ajili ya kulipia hati fungani na dhamana za serikali
zinazoiva.
Aidha,
Mkuya alisema matumizi ya maendeleo yatakuwa Sh trilioni 5.77 sawa na
asilimia 25.9 ya bajeti yote ambapo kiasi cha sh trilioni 4.33 ni fedha
za ndani sawa na asilimia 75 ya fedha za maendeleo na trilioni 1.44
fedha za nje.
"Kwa
kuzingatia sera za uchumi na misingi ya sera za bajeti, sura ya bajeti
inaonesha kuwa Sh trilioni 22.48 zinatarajia kukusanywa, ambapo mapato
ya ndani ya Serikali Kuu yanatarajia kuwa Sh trilioni 14.82 ambayo ni
sawa na asilimia 57.8 ya bajeti yote."
Alisema
serikali inalenga kukusanya mapato ya kodi ya jumla ya Sh trilioni 13.35
sawa na asilimia 90.1 ya mapato ya ndani huku mapato yasiyo ya kodi ni
Sh bilioni 949.2 na yale yatokanayo na vyanzo vya halmashauri
yanatarajia kuwa Sh bilioni 521.9.
Mkuya
alisema Serikali inategemea kukopa kiasi cha Sh trilioni 5.77 kutoka
vyanzo vyenye masharti ya kiabishara huku washirika wa maendeleo
wanatarajiwa kuchangia Sh trilioni 1.89 sawa na asilimia 8.4 ya bajeti,
ikilinganishwa na asilimia 14.8 ya bajeti ya mwaka 2014/15 ambazo sehemu
kubwa ni mikopo ya masharti nafuu. CHANZO: HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment