Home » » KIKWETE ATAKAPONG'ATUKA,ATAKUMBUKWA KWA LIPI?

KIKWETE ATAKAPONG'ATUKA,ATAKUMBUKWA KWA LIPI?

 
 
  Rais Jakaya Mrisho Kikwete
Ingawa aliingia madarakani kwa bashasha nyingi na kauli mbiu zilizotia hamasa, lakini sasa anasema kazi ya urais ni ngumu na anatamani amalize kipindi chake ili awe mtu huru.
 

Hotuba aliyotoa Rais Jakaya Kikwete, Oktoba 2014 alipokuwa Beijing, China ni kama alianza kuwaaga Watanzania  akijiandaa kustaafu urais.
Ingawa aliingia madarakani kwa bashasha nyingi na kauli mbiu zilizotia hamasa, lakini sasa anasema kazi ya urais ni ngumu na anatamani amalize kipindi chake ili awe mtu huru.
“Ni kweli naona kama muda hauendi kwa kasi ya kutosha ili niweze kuwa raia wa kawaida na nipate muda wa kuchunga ng’ombe na mbuzi wangu, nilime mananasi yangu kwa nafasi ya kutosha,” alisema Rais Kikwete alipokuwa  mkutanoni nchini China.
Kama ilivyo ada, kila anayemaliza ngwe yake huacha kumbukumbu. Iwe mbaya au nzuri, swali ni je, yeye atakumbukwa kwa mambo gani? Je, kuna watakaolia kwa furaha kuondoka kwake au watalia kwa majonzi kwamba hawajui kesho yao?
Kikwete atakumbukwa kwa mambo makubwa na mazuri aliyowafanyia Watanzania, lakini vile vile wapo watakaomkumbuka jinsi alivyowaangusha kwa kutenda kinyume cha ahadi zake na kaulimbiu zake za Ari Mpya, Nguvu Mpya, Kasi Mpya au Maisha Bora kwa Kila Mtanzania.
Watanzania wa kada mbalimbali wanazo sababu za kumkumbuka Rais Kikwete atakapong’atuka madarakani. Hii itatokana na jinsi walivyonufaika au kuumizwa kwa namna moja ama nyingine na utawala wake.
Wanawake
 
 Wanawake ni kati ya makundi katika jamii ambayo kwa namna ya pekee watamkumbuka Rais Kikwete kwa jinsi alivyothamini mchango wao na uwezo wao kiutendaji.
Ni katika awamu ya nne tangu ashike wadhifa huo, alipoongeza kasi ya kuwaamini na akawateua kwa wingi baadhi yao kuingia kwenye vyombo vya uamuzi kama uwaziri, ukuu wa mikoa na wilaya na nafasi za uwakilishi kimataifa.
Katika kipindi chake, idadi ya majaji wanawake iliongezeka, ikiwamo hata kufanikisha Anne Makinda kuwa mwanamke wa kwanza kushika nafasi ya juu ya Spika wa Bunge. Je, atawaachia zawadi wanawake kwa kupendekeza mmoja wao kuwa mgombea urais?

Vijana

Kundi hili nalo litakuwa na kila sababu ya kuhuzunika Kikwete atakapoondoka madarakani. Hii ni kwa sababu kila alipofanya uteuzi, hakuwaacha vijana.
Tangu alipojitosa katika kinyang’anyiro cha urais kwa mara ya kwanza mwaka 1995, mkakati wake ulikuwa kuwapa vijana fursa za uongozi na aliposhinda mwaka 2005 aliwateua bila hofu katika nyadhifa mbalimbali.
Mifano ya vijana hawa ni kama January Makamba, Lazaro Nyalandu, Mwigulu Nchemba (uwaziri); Lucy Mayenga, Halima Dendegu, Wilmand Ndilu, Paul Makonda na wengineo (ukuu wa wilaya).

Wazee
 
Mbali na kuendelea kuamini busara za wazee, kila alipotaka kutangaza jambo zito au kutoa hotuba ya mwisho wa mwezi iliyotikisa nchi, alikutana na wazee ama Dar es Salaam au Dodoma, lakini vile vile wazee wamo katika nafasi mbalimbali za uongozi; uwaziri, ukuu wa wilaya na mikoa.

Wazanzibari
Rais Kikwete alijitahidi kadri ya uwezo wake kupatanisha wananchi wa Unguja na Pemba waliotofautiana kwa misingi ya siasa.
Chini ya ushawishi wake Wazanzibari walikubali kuongoza nchi kwa ushirikiano; wakaunda serikali ya Umoja wa Kitaifa. Uhasama uliondoka japokuwa kuna viashiria vya uhasama kurudi.

Wasomi
 
Hakuacha nyuma kundi la wasomi, kwani miongoni mwao ndiyo wanaoongoza wizara nyeti na taasisi mbalimbali. Aliwateua katika nafasi mbalimbali za uongozi japokuwa baadhi yao wamemwangusha.
Atakumbukwa alivyohamasisha ujenzi wa shule za sekondari kukidhi ongezeko kubwa la wanaofaulu kutoka shule za msingi na alivyojenga Chuo Kikuu cha Dodoma, upanuzi wa Chuo Kikuu Huria na vyuo vya kati.

Wanachama wa CCM
 
Tofauti na vyama vingine vya siasa, CCM wanajivunia kumpata mtu aliyekuwa kete ya ushindi kwa vipindi viwili mfululizo 2005—2010 na 2010—2015.
Watamkumbuka alivyowabeba, alivyofanyia marekebisho katiba ya chama kuwa na wajumbe wa Halmashauri Kuu kutoka wilayani, alivyohuisha chama hadi kuwa na mvuto kuliko awali.
Hofu yao ni je, watampata mgombea ambaye atakuwa kete ya ushindi?

Wakulima
 
Kwa mara ya kwanza tangu Serikali ianze kuimba wimbo wa kilimo ni uti wa mgongo, safari hii wakulima na wafugaji walithaminiwa kiasi kwamba walipewa mbolea ya ruzuku, majosho na alitatua migogoro ya ardhi na malisho japo kwa kasi ndogo.

Wananchi
 
Watamkumbuka alivyowapa vyandarua, alivyojenga zahanati, vituo vya afya na alivyoongeza vifaa na majengo katika hospitali kadhaa, hususan katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili; vitengo vya upasuaji wa moyo na vinginevyo.
Kigoma watamfurahia alivyojenga daraja la Mto Malagalasi pamoja na barabara ya kuunganisha na Mkoa wa Tabora; Kusini watamkumbuka alivyokamilisha daraja la Umoja; alivyoongeza vivuko na alivyofurukuta kukamilisha kipande cha kilomita 60 kutoka Ndundu hadi Somanga katika barabara ya Dar es Salaam – Mtwara iliyoanza kujengwa mwaka 1996.

Uchumi
 Rais wa Tanzania Jakaya Mrisho Kikwete akiwa kwenye Mkutano wa Uchumi wa Dunia WEF uliofanyika Davos
Mabadiliko ya sheria ya uwekezaji angalau yamewezesha nchi kuanza kunufaika na kodi ya uzalishaji, ingawa bado si kwa kiasi kikubwa.
Ni katika utawala wa Rais Kikwete ambapo kumekuwa na uboreshaji wa huduma za kibenki, mikopo ya saccos, uboreshaji wa njia za uchukuzi kama barabara, vivuko, reli kwa kununua vichwa na mabehewa, ujenzi na ukarabati wa viwanja vya ndege na uwekezaji umeongezeka.

Vyama vya upinzani:
 
Miongoni mwa watakaolia kwa furaha ni wapinzani wakikumbuka kiongozi huyo alivyoshindwa kujali haki za binadamu na ushahidi ni namna Jeshi la Polisi lilivyotiririsha damu ya wapinzani wake kisiasa.
Mifano mingine ni alivyokimbilia kusuluhisha mgogoro wa Kenya huku polisi wakilaza watu kwa risasi Mtwara kufuatia mgogoro wa gesi; na Serikali yake ilivyoanzisha Operesheni Tokomeza Ujangili iliyoishia kutiririsha damu ya watu wasio na hatia kama wakulima, wafugaji na wawindaji lakini si majangili.

Wanahabari
 Cover Photo
Tasnia nzima ya habari kwa kiasi kikubwa, itamkumbuka Rais Kikwete kwa jinsi Serikali yake ilivyonyonga uhuru wa habari kwa kufungia magazeti kama Mwananchi, MwanaHalisi, Mtanzania, Kulikoni na hivi karibuni The East African na zaidi askari polisi walivyomuua mwanahabari Daudi Mwangosi chini ya utawala wake.
Kubwa zaidi kwa wanahabari ni kushindwa kwake kuwasilisha bungeni muswada wa sheria ya vyombo vya habari na kuondoa sheria kandamizi.

Imeandaliwa na Keneth M Mwandemange kwa msaada wa Gazeti la mwananchi
Toa maoni yako kwa habari hii kwa kuweka email yako hapa,na endelea kutufatilia zaidi Ukurasa wa habari

0 comments:

 
Supported by AMAGA Media services : | |
Copyright © 2015. UKURASA WA HABARI - All Rights Reserved
Templete Designed by Abdallah Magana
Proudly powered by Blogger