Young Killer "Mungu Baba" Official Video Ft. Linah | Ommy Dimpoz | Roma

KIKWETE ATAKAPONG'ATUKA,ATAKUMBUKWA KWA LIPI?

 
 
  Rais Jakaya Mrisho Kikwete
Ingawa aliingia madarakani kwa bashasha nyingi na kauli mbiu zilizotia hamasa, lakini sasa anasema kazi ya urais ni ngumu na anatamani amalize kipindi chake ili awe mtu huru.
 

Hotuba aliyotoa Rais Jakaya Kikwete, Oktoba 2014 alipokuwa Beijing, China ni kama alianza kuwaaga Watanzania  akijiandaa kustaafu urais.
Ingawa aliingia madarakani kwa bashasha nyingi na kauli mbiu zilizotia hamasa, lakini sasa anasema kazi ya urais ni ngumu na anatamani amalize kipindi chake ili awe mtu huru.
“Ni kweli naona kama muda hauendi kwa kasi ya kutosha ili niweze kuwa raia wa kawaida na nipate muda wa kuchunga ng’ombe na mbuzi wangu, nilime mananasi yangu kwa nafasi ya kutosha,” alisema Rais Kikwete alipokuwa  mkutanoni nchini China.
Kama ilivyo ada, kila anayemaliza ngwe yake huacha kumbukumbu. Iwe mbaya au nzuri, swali ni je, yeye atakumbukwa kwa mambo gani? Je, kuna watakaolia kwa furaha kuondoka kwake au watalia kwa majonzi kwamba hawajui kesho yao?
Kikwete atakumbukwa kwa mambo makubwa na mazuri aliyowafanyia Watanzania, lakini vile vile wapo watakaomkumbuka jinsi alivyowaangusha kwa kutenda kinyume cha ahadi zake na kaulimbiu zake za Ari Mpya, Nguvu Mpya, Kasi Mpya au Maisha Bora kwa Kila Mtanzania.
Watanzania wa kada mbalimbali wanazo sababu za kumkumbuka Rais Kikwete atakapong’atuka madarakani. Hii itatokana na jinsi walivyonufaika au kuumizwa kwa namna moja ama nyingine na utawala wake.
Wanawake
 
 Wanawake ni kati ya makundi katika jamii ambayo kwa namna ya pekee watamkumbuka Rais Kikwete kwa jinsi alivyothamini mchango wao na uwezo wao kiutendaji.
Ni katika awamu ya nne tangu ashike wadhifa huo, alipoongeza kasi ya kuwaamini na akawateua kwa wingi baadhi yao kuingia kwenye vyombo vya uamuzi kama uwaziri, ukuu wa mikoa na wilaya na nafasi za uwakilishi kimataifa.
Katika kipindi chake, idadi ya majaji wanawake iliongezeka, ikiwamo hata kufanikisha Anne Makinda kuwa mwanamke wa kwanza kushika nafasi ya juu ya Spika wa Bunge. Je, atawaachia zawadi wanawake kwa kupendekeza mmoja wao kuwa mgombea urais?

Vijana

Kundi hili nalo litakuwa na kila sababu ya kuhuzunika Kikwete atakapoondoka madarakani. Hii ni kwa sababu kila alipofanya uteuzi, hakuwaacha vijana.
Tangu alipojitosa katika kinyang’anyiro cha urais kwa mara ya kwanza mwaka 1995, mkakati wake ulikuwa kuwapa vijana fursa za uongozi na aliposhinda mwaka 2005 aliwateua bila hofu katika nyadhifa mbalimbali.
Mifano ya vijana hawa ni kama January Makamba, Lazaro Nyalandu, Mwigulu Nchemba (uwaziri); Lucy Mayenga, Halima Dendegu, Wilmand Ndilu, Paul Makonda na wengineo (ukuu wa wilaya).

Wazee
 
Mbali na kuendelea kuamini busara za wazee, kila alipotaka kutangaza jambo zito au kutoa hotuba ya mwisho wa mwezi iliyotikisa nchi, alikutana na wazee ama Dar es Salaam au Dodoma, lakini vile vile wazee wamo katika nafasi mbalimbali za uongozi; uwaziri, ukuu wa wilaya na mikoa.

Wazanzibari
Rais Kikwete alijitahidi kadri ya uwezo wake kupatanisha wananchi wa Unguja na Pemba waliotofautiana kwa misingi ya siasa.
Chini ya ushawishi wake Wazanzibari walikubali kuongoza nchi kwa ushirikiano; wakaunda serikali ya Umoja wa Kitaifa. Uhasama uliondoka japokuwa kuna viashiria vya uhasama kurudi.

Wasomi
 
Hakuacha nyuma kundi la wasomi, kwani miongoni mwao ndiyo wanaoongoza wizara nyeti na taasisi mbalimbali. Aliwateua katika nafasi mbalimbali za uongozi japokuwa baadhi yao wamemwangusha.
Atakumbukwa alivyohamasisha ujenzi wa shule za sekondari kukidhi ongezeko kubwa la wanaofaulu kutoka shule za msingi na alivyojenga Chuo Kikuu cha Dodoma, upanuzi wa Chuo Kikuu Huria na vyuo vya kati.

Wanachama wa CCM
 
Tofauti na vyama vingine vya siasa, CCM wanajivunia kumpata mtu aliyekuwa kete ya ushindi kwa vipindi viwili mfululizo 2005—2010 na 2010—2015.
Watamkumbuka alivyowabeba, alivyofanyia marekebisho katiba ya chama kuwa na wajumbe wa Halmashauri Kuu kutoka wilayani, alivyohuisha chama hadi kuwa na mvuto kuliko awali.
Hofu yao ni je, watampata mgombea ambaye atakuwa kete ya ushindi?

Wakulima
 
Kwa mara ya kwanza tangu Serikali ianze kuimba wimbo wa kilimo ni uti wa mgongo, safari hii wakulima na wafugaji walithaminiwa kiasi kwamba walipewa mbolea ya ruzuku, majosho na alitatua migogoro ya ardhi na malisho japo kwa kasi ndogo.

Wananchi
 
Watamkumbuka alivyowapa vyandarua, alivyojenga zahanati, vituo vya afya na alivyoongeza vifaa na majengo katika hospitali kadhaa, hususan katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili; vitengo vya upasuaji wa moyo na vinginevyo.
Kigoma watamfurahia alivyojenga daraja la Mto Malagalasi pamoja na barabara ya kuunganisha na Mkoa wa Tabora; Kusini watamkumbuka alivyokamilisha daraja la Umoja; alivyoongeza vivuko na alivyofurukuta kukamilisha kipande cha kilomita 60 kutoka Ndundu hadi Somanga katika barabara ya Dar es Salaam – Mtwara iliyoanza kujengwa mwaka 1996.

Uchumi
 Rais wa Tanzania Jakaya Mrisho Kikwete akiwa kwenye Mkutano wa Uchumi wa Dunia WEF uliofanyika Davos
Mabadiliko ya sheria ya uwekezaji angalau yamewezesha nchi kuanza kunufaika na kodi ya uzalishaji, ingawa bado si kwa kiasi kikubwa.
Ni katika utawala wa Rais Kikwete ambapo kumekuwa na uboreshaji wa huduma za kibenki, mikopo ya saccos, uboreshaji wa njia za uchukuzi kama barabara, vivuko, reli kwa kununua vichwa na mabehewa, ujenzi na ukarabati wa viwanja vya ndege na uwekezaji umeongezeka.

Vyama vya upinzani:
 
Miongoni mwa watakaolia kwa furaha ni wapinzani wakikumbuka kiongozi huyo alivyoshindwa kujali haki za binadamu na ushahidi ni namna Jeshi la Polisi lilivyotiririsha damu ya wapinzani wake kisiasa.
Mifano mingine ni alivyokimbilia kusuluhisha mgogoro wa Kenya huku polisi wakilaza watu kwa risasi Mtwara kufuatia mgogoro wa gesi; na Serikali yake ilivyoanzisha Operesheni Tokomeza Ujangili iliyoishia kutiririsha damu ya watu wasio na hatia kama wakulima, wafugaji na wawindaji lakini si majangili.

Wanahabari
 Cover Photo
Tasnia nzima ya habari kwa kiasi kikubwa, itamkumbuka Rais Kikwete kwa jinsi Serikali yake ilivyonyonga uhuru wa habari kwa kufungia magazeti kama Mwananchi, MwanaHalisi, Mtanzania, Kulikoni na hivi karibuni The East African na zaidi askari polisi walivyomuua mwanahabari Daudi Mwangosi chini ya utawala wake.
Kubwa zaidi kwa wanahabari ni kushindwa kwake kuwasilisha bungeni muswada wa sheria ya vyombo vya habari na kuondoa sheria kandamizi.

Imeandaliwa na Keneth M Mwandemange kwa msaada wa Gazeti la mwananchi

MAGAZETI LEO ALHAMISI



    Na Awadh Ibrahim

     

    BAJETI YA MWISHO YA RAIS KIKWETE YAWASILISHWA


       Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum
      Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum.

      SERIKALI imewasilisha mwelekeo wa bajeti kwa Kamati ya Bunge, ambayo inalenga zaidi kupeleka umeme na huduma za maji vijijini, kumalizia miradi ambayo haijakamilika na kutenga fedha kwa ajili ya uchaguzi mkuu ujao.
      Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum alisema wanaandaa bajeti ambayo itasaidia kumaliza mambo yote waliyoahidi, ambayo yameainishwa kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambayo serikali iliahidi wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita.
      "Bajeti ya mwaka 2015/16 ni ya kipekee. Ni mwaka wa uchaguzi, ni mwaka ambao serikali ya Awamu ya Nne inamaliza muda wake na serikali mpya kuingia madarakani. "Ni mwaka ambao Mkukuta na Mpango wa Kwanza wa Maendeleo ya Milenia ya miaka mitano inafikia tamati, Malengo ya Milenia ya mwaka 2015 yanafikia ukomo na pia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2010 unakamilika," alisema.
      Vipaumbele vya bajeti
      Akiwasilisha mwelekeo wa bajeti hiyo kwa wabunge jijini Dar es Salaam jana, Mkuya alisema bajeti ya mwaka huu imejikita zaidi kutathmini na kuangalia changamoto kwenye sekta ya maji, nishati, rasilimaliwatu na kumalizia miradi ambayo haijakamilika.
      "Vipaumbele kwenye bajeti hii vimejikita zaidi kwenye kuandaa awamu ya pili ya Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano utakaoanza Juni mwaka 2016, na mkazo zaidi ni kwenye miradi ya umeme vijijini, maji vijijini, kuimarisha rasilimaliwatu na kugharamia uchaguzi mkuu," alisema Mkuya.
      Akifafanua, alisema katika mwelekeo huo wa Bajeti mpya ya mwaka 2015/16, jumla ya Sh takribani trilioni 23 zinatarajiwa kukusanywa na kutumika katika matumizi ya maendeleo na ya kawaida.
      Alisema katika matumizi ya maendeleo,vipaumbele vitano ambavyo vimetajwa hapo juu (maji, umeme, rasilimaliwatu, kumalizia miradi viporo na kugharamia uchaguzi mkuu). Jumla ya fedha zilizotengwa ni Sh trilioni 5.8.
      Mchanganuo wake ni kwamba fedha za ndani ni Sh trilioni 4.3 na fedha za nje ni Sh trilioni 1.4 ambazo kwa ujumla zitatumika kwenye utekelezaji wa vipaumbele vilivyoainishwa na kumalizia miradi ambayo haikukamilika kwenye bajeti iliyopita.
      Katika sekta ya nishati, kipaumbele kimewekwa katika kuendeleza miradi ya umeme vijijini, ambapo hadi sasa wateja 2,602 wa vijijini kwenye mikoa ya Simiyu, Singida, Kagera,Tanga, Ruvuma na Iringa, wameunganishiwa umeme.
      Aidha, katika sekta ya maji vijijini, tathmini ya bajeti iliyopita, inaonesha kuwa jumla ya miradi ya maji vijijini, ilikuwa 123 iliyojengwa na kukamilika na idadi hiyo imewanufaisha wananchi 463,750.
      Katika bajeti hii, mkazo umewekwa katika kukamilisha miradi ya maji vijijini ambayo haijakamilika, ikiwemo miradi ya ujenzi wa mabwawa ya Kawa mkoani Rukwa, Bwawa la Sasajila lililopo Dodoma na bwawa la Mwanjoro lililopo Shinyanga pamoja na miradi mingine kwenye maeneo mengine vijijini.
      Akizungumzia suala la Uchaguzi Mkuu, unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu, ambalo ni moja ya vipaumbele katika bajeti hiyo mpya, Mkuya alisema bajeti imejikita katika kugharamia uchaguzi huo ili ufanyike na kupata serikali mpya itakayoendelea kutekeleza bajeti hii.
      Mwelekeo wa bajeti
      Akizungumzia mwelekeo wa bajeti, Mkuya alisema Serikali imepanga kutumia Sh trilioni 22.48 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo katika bajeti ya mwaka 2015/16 huku utegemezi wa fedha za kigeni ukipungua kutoka asilimia 14.8 ya mwaka wa fedha uliopita hadi asilimia 8.4 kwa mwaka ujao wa fedha.
      Bajeti ya mwaka 2014/15 ilikuwa ni Sh trilioni 19.9, hivyo mwelekeo wa bajeti hiyo inakuwa na ongezeko kwa takribani asilimi 16.
      Alisema katika fedha hizo, sh trilioni 16.71 zimetengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida, ikijumuisha Sh trilioni 6.61 kwa ajili ya mishahara ya watumishi wa Serikali na taasisi, Sh trilioni 3.41 kwa ajili ya matumizi mengineyo ya Wizara huku mikoa ikiwa ni Sh bilioni 83.55 na Mamlaka za Serikali za Mitaa ni Sh bilioni 208.75 wakati Sh trilioni 2.60 zikitengwa kwa ajili ya kulipia hati fungani na dhamana za serikali zinazoiva.
      Aidha, Mkuya alisema matumizi ya maendeleo yatakuwa Sh trilioni 5.77 sawa na asilimia 25.9 ya bajeti yote ambapo kiasi cha sh trilioni 4.33 ni fedha za ndani sawa na asilimia 75 ya fedha za maendeleo na trilioni 1.44 fedha za nje.
      "Kwa kuzingatia sera za uchumi na misingi ya sera za bajeti, sura ya bajeti inaonesha kuwa Sh trilioni 22.48 zinatarajia kukusanywa, ambapo mapato ya ndani ya Serikali Kuu yanatarajia kuwa Sh trilioni 14.82 ambayo ni sawa na asilimia 57.8 ya bajeti yote."
      Alisema serikali inalenga kukusanya mapato ya kodi ya jumla ya Sh trilioni 13.35 sawa na asilimia 90.1 ya mapato ya ndani huku mapato yasiyo ya kodi ni Sh bilioni 949.2 na yale yatokanayo na vyanzo vya halmashauri yanatarajia kuwa Sh bilioni 521.9.
      Mkuya alisema Serikali inategemea kukopa kiasi cha Sh trilioni 5.77 kutoka vyanzo vyenye masharti ya kiabishara huku washirika wa maendeleo wanatarajiwa kuchangia Sh trilioni 1.89 sawa na asilimia 8.4 ya bajeti, ikilinganishwa na asilimia 14.8 ya bajeti ya mwaka 2014/15 ambazo sehemu kubwa ni mikopo ya masharti nafuu. CHANZO: HABARI LEO

      BOTI YA TANZANIA YANASWA NA UNGA SCOTLAND

      Boti ya Hamal (yenye rangi nyekundu) ikiwa chini ya ulinzi baada ya kukamatwa na boti ya polisi wa Scotland
      Boti ya Hamal (yenye rangi nyekundu) ikiwa chini ya ulinzi baada ya kukamatwa na boti ya polisi wa Scotland

      BOTI yenye usajili wa Tanzania, imekamatwa kwenye Bahari ya Kaskazini na baada ya kupekuliwa katika bandari ya Arberdeen huko Scotland, imekutwa na shehena ya dawa zakulevya.  
      Kwa mujibu wa mtandao wa BBC, boti hiyo inayoitwa Hamal, yenye urefu wa mita 32 na uwezo wa kubeba tani 422, ilizuiwa Alhamisi na vyombo viwili vya ulinzi vinavyofanya doria ikiwa umbali wa maili 100 kutoka usawa wa bahari mashariki mwa mji wa Arberden.
      Kwa mujibu wa mtandao unaoonyesha vilipo vyombo vya baharini, katikati ya Februari,  boti hiyo ilikuwa Uturuki na wiki mbili zilizopita ilianza safari kutoka visiwa vya Tenerife huko Hispania na ilipokamatwa ilikuwa inaelekea Hamburg, mji wa pili kwa ukubwa wa Ujerumani ikitazamiwa kufika usiku wa Ijumaa iliyopita.
      Boti hiyo imekutwa na watu 9 wenye umri kati ya miaka 26 na 63 na wameshtakiwa kwa kukutwa na dawa za kulevya wakitarajiwa kupelekwa mahakamani. Hata hivyo watu hao utaifa wao haukuweza kupatikana mara moja.
      John McGowan wa mamlaka inayoshughulikia uhalifu kitengo cha ulinzi wa mipaka (NCA-BPC), amesema boti hiyo imekamatwa na kiwango kikubwa cha dawa za kulevya na kukamatwa kwake kumewezekana kutokana na ushirikiano wa taasisi za ulinzi za Uingereza na ushiriiano wa kimataifa.
      “Kiasi kamili cha dawa hizo bado hakijafahamika na upekuaji bado unaendelea kwa ushirikiano wa NCA na Jeshi la Polisi ya Scotland,” amesema.
      Chanzo:Mwanahalisi Online

      KAFULILA APATA TUZO YA KUFICHUA ESCROW


      Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila akipokea tuzo ya Utetezi wa Haki za Binadamu kutoka kwa THRD
       
       
      Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila akipokea tuzo ya Utetezi wa Haki za Binadamu kutoka kwa THRD
       
      DAVID Kafulila-Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), ametunukiwa tuzo na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu nchini (THRD), akiwa miongoni mwa watu watatu ambao wamefanya kazi katika mazingira magumu kwa lengo la kutetea haki mwaka 2014.  
      Pamoja na Kafulila, wengine ni aliyekuwa mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba kutoka kundi la 201 akiwakilisha Zanzibar, Salma Said na Mkurugenzi wa Baraza la Wanawake Wafugaji kutoka Loliondo, Maanda Ngoitiko.
      Akizungumza na MwanaHALISIOnline, Mratibu wa THRD, Onesmo Ole Ngurumwa amesema watu hao ni wale “waliofanya kazi ya kutetea haki za binadamu katika mazingira magumu huku wakitishiwa kuuwawa lakini kazi zao zimesaidia kuleta mabadiliko”.
      “Nawasihi watu waendelee kupigania haki. Licha ya kwamba wanatishwa na hata wengine kuuwawa, wanapaswa kusimamia kile wanachokiamini ambacho ni haki,” amesema Olengurumwa
      Ameongeza kuwa, maaadhimisho haya ni ya pili kufanyika Tanzania ambapo kwa mara ya kwanza yalifanyika mwaka 2013.
      Ametaka siku hii itambuliwe kimataifa na isiwe nchini tu, huku akisisitiza kwamba wanaofanya utetezi huo waangalie usalama wao katika harakati za kupigania haki za wengine.
      Naye Ernest Sungura, Mkurugenzi wa Mfuko wa Vyombo vya Habari Tanzania (TMF), amesema katika kuelekea katika uchaguzi mkuu, wanahabari wanatakiwa kulindwa na vyombo vinavyoweza kudhamiria kuwakingia kifua kutokana na wao kuandika habari za uchunguzi ambazo mara kwa mara zimeonekana kugusa maslahi ya watu mbalimbali moja kwa moja.
      Wawakilishi kutoka nchi za Umoja wa Ulaya nchini na washauri wa masuala ya haki za binadamu katika nchi za Umoja wa Mataifa, wameeleza kuwa, kama Serikali haithamini haki za mtu mmoja mmoja ipo hatari kubwa ya kupoteza nguvu kazi ya taifa kwa jambo ambalo lingeweza kutatuliwa kwa njia rahisi.
      Balozi wa Jumuiya ya Ulaya chini, Filberto Sebrregondi, amesema umefika wakati wa kila mwananchi kutambua kuwa wimbi la kuminywa haki za watu wasio na uwezo linakuwa kwa kasi nchini, licha ya kubainisha kwamba amefurahishwa kwa namna washiriki walivyoonyesha ushirikiano kwa mwamvuli wa mitandao hiyo ya kutetea haki za binadamu.
      Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk.Helen Kijo-Bisimba, akiongea katika maadhimisho hayo, alisisitiza kwamba haki za binadamu ndizo zinazowafanya wanadamu waishi na kwamba mtu yeyote asipofanya utetezi wa haki za binadamu anataka ubinadamu wa wengine uishie njia panda.
      Kwa upande wake, Kafulia ambaye amepewa tuzo hiyo kwa kuibua bungeni kashfa ya ufisadi wa Sh. 306 bilioni katika akaunti ya Tegeta Escrow, ameliambia MwanaHALISIOnline kuwa “tuzo hii imenipa ujasiri zaidi katika kusimamia maslahi ya taifa katika vita vya ufisadi. Inaonesha katika mapambano haya sipo peke yangu”.
      “Ni mara yangu ya kwanza kuingia bungeni. Tena nikiwa kijana. Hakuna mbunge aliyewahi kukabidhiwa tuzo hii hasa kwa kazi niliyoifanya ya kuibua ufisadi wa akaunti ya Tegeta Escrow. Inaonesha vijana tunaweza. Japo ilikuwa ni kazi hatari na wakati mwingine nilitishiwa maisha yangu,” amesema Kafulila.
      Ameupongeza mtanda wa THRD na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kwa ushauri wa kisheria waliompa wakati akitoa ushahidi wa ufisadi wake kwenye mamlaka za uchunguzi na hata alipofunguliwa kesi na Seth Herbinder Singh, mmoja wa wanufaika wa fedha za Escrow.
      Naye Salma Said, alitishiwa maisha baada ya kuonesha msimamo wake hadharani wa kupinga Rasimu ya Katiba inayopendekezwa akisema “ni kinyume na maoni yalitotolewa na wananchi” huku Ngoitiko akiwa ni mtetezi wa haki za binadamu vijijini hasa wafugaji walionyang’anywa maeneo yao Loliondo mkoani Arusha.
      Tuzo hizo zimejumuisha cheti cha kutambua mchango wa kupigania haki na ngao ambayo ni alama ya ushujaa.
      Maadhimisho hayo yameenda sambamba na maonyesho ya watetezi hao, ambao ni Kampuni ya Jamii Media (Wamiliki wa mitandao maarufu ya kijamii nchini ya FikraPevu.com na JamiiForums, TGNP Mtandao, TAMWA, LHRC, HAKI ARDHI INSTITUTE, JUKWAA LA KATIBA, TAWLA, SIKIKA, ZLSC, TAS, TACOSODE, TANLAP, LEAT,Human Rights Comission, TVVA, Haki Catalyst, German Foundation, German Embasy, SANA, na CESOPE.

      MBEYA DERBY: MBEYA CITY MTUSAMEHE KICHAPO KIPO PALE PALE





                 
       
      Zikiwa zimesalia siku mbili Mtanange wa Ligi kuu Tanzania bara kupigwa katika dimba

      293 WAOKOLEWA NCHINI NIGERIA KUTOKA KAMBI ZA BOKO HARAM

      Jeshi la Nigeria
      Jeshi la Nigeria limesema limewaokoa watoto wa kike mia mbili na akina mama tisini na tatu kutoka katika kambi ya Boko Haram iliyoko katika msitu wa Sambisa, kaskazini mashariki mwa nchi hiyo. Jeshi hilo limesema watoto hao waliokolewa si kati ya wale waliotekwa mwaka mmoja uliopita na kundi la kiislamu katika eneo la Chibok.
      Jeshi limeiambia BBC kwamba wanawake na watoto hao wa kike walikutwa katika kambi nne tofauti ambapo silaha pia zimekamatwa,Msemaji wa jeshi amesema waliwapata wasichana hao baada ya kuziharibu kambi hizo.
      "ni muda mfupi tu uliopita, wanajeshi wetu wameingia katika msitu wa Sambisa, kutokea upande wa Alafa, ambapo walikuta kambi nne zinazomilikiwa na wapiganaji na kuziharibu, hapo ndipo walipogundua kuwa kuna wasichana wapatao mia mbili na wanawake tisini na tatu."
       
      Jeshi la Nigeria
      Kwa sasa jeshi limezuiwa kutoa utambulisho wa wasichana hao. Hata hivyo, jeshi limethibitisha kwamba wasichana hao sio wale wanafunzi waliotekwa katika mji wa Chibok.
      "tuko katika mchakato wa kuwachunguza hawa wasichana ili tuweze kubaini utambulisho wao, lakini kitu kimoja nataka nikiweke wazi kwa umma, tunapotaja idadi ya wasichana mia mbili, tayari watu wanaanza kufikiria wasichana mia mbili wa Chibok waliotekwa mwaka jana, hawa sio wasichana wa Chibok, tutaendelea kuwajuza kadri muda unavyokwenda iwapo kutakuwa na taarifa zozote. "
      Credit:BBC
       
      Supported by AMAGA Media services : | |
      Copyright © 2015. UKURASA WA HABARI - All Rights Reserved
      Templete Designed by Abdallah Magana
      Proudly powered by Blogger