Home » » BOKO HARAM YATEKA NYARA MAMIA YA WANAWAKE NA WATOTO NCHINI NIGERIA

BOKO HARAM YATEKA NYARA MAMIA YA WANAWAKE NA WATOTO NCHINI NIGERIA


Kutekwa nyara na Boko Haram mamia ya wanawake na watoto nchini Nigeria 

Wanamgambo wa kundi la kigaidi la Boko Haram nchini Nigeria wamewateka nyara wanawake na watoto mia nne katika shambulio walilofanya mapema mwezi huu kwenye mji wa Damasak ulioko kilomita kadhaa kutoka kwenye mpaka wa pamoja wa nchi hiyo na Chad. Mji huo wa kaskazini mashariki mwa Nigeria uliokuwa ukishikiliwa na kundi la Boko Haram ulikombolewa na jeshi la nchi hiyo siku kumi zilizopita. Kwa mujibu wa mashuhuda, wanamgambo wa kundi la Boko Haram waliwaua watu 50 miongoni mwa mateka hao kabla ya kurejea nyuma kwenye ngome zao. Hadi sasa hakuna taarifa za uhakika kuhusu hatima ya mateka waliosalia. Tangu kundi la kigaidi la Boko Haram lilipoanzisha mashambulio yake ndani ya ardhi ya Nigeria mwaka 2009, makumi ya maelfu ya watu wameuawa na wengine zaidi ya milioni moja wamelazimika kuyahama makaazi yao. Kutokana na kuendelea mashambulio ya kundi hilo katika miaka ya hivi karibuni, na kushindwa jeshi la Nigeria kukabiliana na mashambulio hayo, hatimaye mnamo tarehe 14 ya mwezi uliopita wa Februari, Nigeria yenyewe pamoja na Chad na Niger zilianzisha operesheni za pamoja za mashambulio dhidi ya Boko Haram. Muungano huo wa kieneo uliongeza matumaini ya kulitokomeza kundi hilo la kigaidi. Viongozi wa Nigeria wametangaza hivi karibuni kuwa miji 38 ya kaskazini mashariki imekombolewa, na magaidi wa Boko Haram wametimuliwa kutoka kwenye majimbo kadhaa waliyokuwa wakiyashikilia hususan jimbo la Borno. Huku ripoti zikieleza kuhusu kufurushwa na kurudi nyuma kundi la Boko Haram

kutoka maeneo yaliyokuwa yakishikiliwa na kundi hilo, kutangazwa ghafla habari ya kutekwa nyara idadi kubwa ya wanawake na watoto kumewatia hofu na mshtuko wananchi wa Nigeria. Kuibuka tena habari za shambulio na utekaji nyara uliofanywa na kundi la kigaidi la Boko Haram kumejiri wakati siku chache nyuma Rais Goodluck Jonathan wa Nigeria alikuwa ametangaza kwamba kundi hilo litakuwa limekwisha sambaratishwa ndani ya kipindi cha mwezi mmoja. Akizungumza kwa matumaini makubwa alisema hautopindukia muda wa mwezi mmoja kabla ya Boko Haram kutimuliwa na kutolewa nje ya ardhi ya Nigeria. Rais wa Nigeria alitilia nguvu madai yake hayo kwa kuashiria kukombolewa vijiji na maeneo kadhaa katika kipindi cha wiki zilizopita kwa msaada wa majeshi ya nchi jirani, yaani Chad, Cameroon, Niger na Benin. Kwa muda mrefu, wananchi wa Nigeria wamekuwa wakimshutumu kiongozi wao huyo kwamba anaonyesha ulegevu katika kukabiliana na kundi la Boko Haram. Bali kuna hata wale waliokwenda mbali zaidi kwa kutamka kwamba Rais Jonathan anawaunga mkono nyuma ya pazia magaidi hao. Wapinzani wa serikali wanaeleza kwamba Jonathan analiunga mkono kwa siri kundi la kigaidi la Boko Haram kwa shabaha ya kuwadhoofisha Waislamu. Lakini madai yote hayo ya wapinzani yanapingwa na waungaji mkono wa kiongozi huyo. Itakumbukwa kuwa mnamo siku kadhaa nyuma, kwa mara ya kwanza, Rais wa Nigeria alikiri kwamba serikali yake haikuichukulia kwa uzito unaostahiki hatari ya kundi la Boko Haram na hivyo kuandaa suhula chache kwa ajili ya kupambana na kundi hilo. Kwa mtazamo wa wataalamu wa mambo tukio la kutekwa nyara idadi kubwa ya wanawake na watoto litaathiri nafasi ya Rais Jonathan katika uchaguzi mkuu ujao wa Nigeria. (CHANZO:Idhaa ya Kiswahili Radio Tehran)
Toa maoni yako kwa habari hii kwa kuweka email yako hapa,na endelea kutufatilia zaidi Ukurasa wa habari

0 comments:

 
Supported by AMAGA Media services : | |
Copyright © 2015. UKURASA WA HABARI - All Rights Reserved
Templete Designed by Abdallah Magana
Proudly powered by Blogger