Home » » WABUNGE CCM SASA NJIAPANDA

WABUNGE CCM SASA NJIAPANDA


 
Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi  ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (Takukuru), Dk  Edward Hoseah akitoa mada kwenye semina ya wabunge iliyofanyika Dodoma jana. Picha na Emmanuel Herma
Share
Dar/Dodoma. Wakati mkutano wa mwisho wa Bunge la 10 ukiendelea, baadhi ya wabunge CCM wamebaki njiapanda kimaamuzi iwapo waendelee kuikosoa Serikali ya chama chao na kujiweka mahali pazuri kwa wapigakura wao au waifagilie Serikali bila ya kujali hatima ya ubunge wao.
Mkutano huu wa Bajeti utamalizika kwa Bunge kuvunjwa na wabunge kwenda kwenye Uchaguzi Mkuu, hali inayowafanya baadhi yao kuamua kukwepa vikao ‘kuimarisha majimbo yao’ na wengine kulalamika hata kufikisha madai yao kwenye Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).
Wakati hali ikiwa hivyo, wenzao wa upinzani wameamua kutumia fursa hiyo kuisulubu Serikali kwa tuhuma na kashfa mbalimbali za nyuma na upungufu wake sasa ikiwamo uandikishaji Daftari la Wapigakura, kuahirishwa Kura ya Maoni, sakata la escrow na dosari zilizotokana katika utekelezaji wa bajeti za maendeleo katika bajeti iliyopita ya mwaka 2014/15.
Hali hiyo inakuja wakati joto la uchaguzi likiwa limepanda huku wapigakura wakiwa na hamu kusikia wawakilishi wao wamevuna kitu gani na jinsi gani wanaiwajibisha Serikali lakini, wawakilishi hao wakitakiwa kuisafisha Serikali ili kukiwekea chama chao mazingira mazuri katika uchaguzi wa Oktoba 25.
Tangu kuanza kwa vikao vya bajeti, wachambuzi wa masuala ya kisiasa wanasema ni wabunge wachache tu wa CCM ambao wameonekana kuitetea Serikali dhidi ya tuhuma zinazoibuliwa, tofauti na ilivyokuwa katika mikutano iliyopita.
Pamoja na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye kuwa mstari wa mbele kukemea udhaifu wa watendaji wa Serikali, baadhi ya wabunge wanahofia kukatwa majina yao endapo wataiwajibisha Serikali ya chama chao.
Hata hivyo, baadhi ya wabunge wanaonekana kutoyumba na kuendelea na msimamo wao wa kuikosoa na kuiwajibisha Serikali, wakiwamo Mbunge wa Kahama (CCM), James Lembeli ambaye amenukuliwa akilalamika kutishiwa kukatwa jina na viongozi wa chama hicho, Ester Bulaya (Viti maalumu) na Mbunge wa Ludewa, Deo Filikunjombe na Kangi Lugola wa Mwibara.
Mtazamo wa kisomi
Mhadhiri Mwandamizi wa Sayansi ya Siasa, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Alexander Makulilo alisema kila chama cha siasa huwa kinaweka ajenda ya uwajibikaji wa pamoja kwa masilahi ya chama hicho.
Dk Makulilo alisema siyo Tanzania pekee, bali hata vyama vingine tawala barani Afrika na Uingereza, vimekuwa na utaratibu wa kukubaliana mambo ya kusimamia kauli ya pamoja.
“Kuna kitu kinaitwa ‘party discipline’ ndani ya chama lakini kuna mambo wanayoweza kuyaacha yajadiliwe kwa uhuru wa kila mbunge na kuna mambo ambayo lazima waonyeshe msimamo wa pamoja,” alisema na kuongeza:
“Sasa wabunge wanaweza kuwa kwenye wakati mgumu kama msimamo wa chama unakinzana na mtazamo wa wapigakura wa mbunge fulani. Hata hivyo, bado kwa siasa ya Tanzania haiwezi kuwa kikwazo cha kukosa ubunge kwani wengi hutumia rushwa zaidi.”

Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba Tanzania(Jukata), Deus Kibamba alisema licha ya ujasiri kwa baadhi ya wabunge wa CCM, wengine wamekuwa na hofu ya kukatwa majina.
“Kitanzi kikubwa kilichopo, huwezi kuwa mbunge mpaka ukubalike ndani ya CCM, lakini mwaka 2010 walikata majina wabunge wengi matokeo yake wananchi wakachagua upinzani, yaani chama kilichagua wagombea ambao ni tofauti na chaguo lao.
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), ambaye ni Mkuu wa kitengo cha Sayansi ya Siasa, Emmanuel Mallya alisema hali ilivyo kwa sasa ni lazima mbunge atazame upepo wa pande zote mbili hususan ndani jimbo lake.
“Hakuna mbunge anayetaka kwa sasa kuonekana akitetea mambo yasiyokubalika kwa wapigakura wake iwapo anahitaji kuomba kura tena, lakini kama hana shida ya kurudi jimboni, basi anaweza kuishambulia Serikali kwa vyovyote au kuisifia kwa namna yoyote,” alisema na kuongeza: “Kuhusu kuadhibiwa na chama chake hiyo haiwezekani kwani hata CCM wanapima hoja na kuangalia upepo wa kukubalika kwa mtu jimboni.”
Hata hivyo, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba (Viti Maalumu -CCM), alisema haoni mazingira magumu kwa mbunge wa CCM kuitetea Serikali kwani ni maoni yake huru yanayohitaji kuheshimiwa.
“Bunge ni mapambano kati ya upinzani na CCM, lakini suala la kuikosoa Serikali liko palepale kwa wabunge wa CCM na ndiyo maana tunaishauri, kuikumbusha na kisha tunaunga mkono kwa kuamini Serikali ijayo itashughulikia kero za wananchi zilizobakia jimboni,” alisema Simba.
Nape alisema siyo kweli kwamba wabunge wa CCM ndiyo wamekuwa na wakati mgumu, bali wamekuwa huru kuiwajibisha Serikali na ndiyo maana wamekuwa wakiibua tuhuma mbalimbali za ufisadi.
“Kwa hivyo siyo sawa kabisa kusema wabunge wa CCM wana wakati mgumu, mbona hamsemi kuhusu tuhuma za wabunge wa upinzani kwenye majimbo yao?” alisema Nape na kuongeza:
“Asilimia 78 ya wabunge ni wa CCM lakini wanaruhusu na kuibua ufisadi, kama wangekuwa na wakati mgumu wangekuwa wanapitisha? Siyo sawa kabisa kujenga mtazamo huo.”
Wamlilia Dk Hoseah
Katika hatua nyingine, baadhi ya wabunge wa CCM jana walimlilia Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk Edward Hosea wakitaka awasaidie kukomesha rafu na rushwa zinavyofanywa na wenyeviti wa chama hicho wa wilaya
na baadhi ya viongozi wa Serikali.

Walitoa kilio hicho kwenye semina ya wabunge iliyoandaliwa na Chama cha Wabunge cha Kupambana na Rushwa (APNAC) mjini Dodoma na kuhudhuriwa na wabunge baadhi ya mawaziri.
Wakichangia katika semina hiyo wabunge hao walisema rafu na rushwa zimekuwa zikifanyika hadharani majimboni miezi mitatu iliyopita.
Mbunge wa Nkasi Kusini (CCM), Desderius Mipata alisema alitoa taarifa kwa Takukuru kuhusu mmoja ya kiongozi wa Serikali  kujihusisha na kampeni kabla ya muda lakini hajapata mrejesho.
“Huyu anatumia gari, mafuta na dereva wa Serikali kuzunguka vijijini katika jimbo langu. Hivi mimi sina haki ya kujua kinachoendelea maana ninayemtuhumu anapata taarifa kutoka makao makuu juu ya yanayoendelea.”
Mbunge wa pili kulalamika ni wa Igalula, (CCM), Dk Athuman Mfutakamba aliyesema mwenyekiti wa CCM wilayani kwake ambaye ameonyesha nia ya kugombea katika jimbo lake ameanza kugawa sare kwa kisingizio kuwa anatekeleza ahadi zake... “Takukuru mfike na huko muangalie yanayofanyika kwa kisingizio cha kutekeleza ahadi..”
Pia alisema kuna mgombea ambaye alimshinda katika kura za maoni mwaka 2010, ameanzisha vikundi vya kusaidia wanawake na vijana.
“Huyu naye aangaliwe kwa sababu mimi ninaamini kuwa hiyo ni rushwa,” alisema.
Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Abia Nyabakari alisema mwenyekiti wa CCM wa wilaya (hakuitaja) alimpigia simu na kumweleza kuwa amemwona akipitapita katika jimbo la Manyovu wilayani Kasulu akiwa na gari lake la kijani.
“Nilimwambia mimi hata sipo huko anakosema lakini aliendelea kunieleza kuwa nifahamu hilo jimbo ni la Obama (Mbunge wa sasa Albert Obama Ntabaliba,” alilalamika.
Alisema Januari 26 mwaka huu kulifanyika kikao cha halmashauri ya wilaya na kiongozi mmoja aliwaambia wajumbe kuwa amepewa fedha na mama mmoja kwa ajili ya kuwanunulia chakula.
Alisema baada ya kula aliwaambia wajumbe wahakikishe mama huyo anapita na kuonya atakayezuia mama hiyo kupita maana ataadhibiwa hata kupoteza uanachama.
“Alisema atakayemzuia mama huyo kupita katika ubunge atahakikisha hafiki popote, ikiwezekana hata kufutiwa uanachama. Mimi ninatishwa na yeye ni kiongozi wa kuidhinisha wagombea,” alisema.

Hata hivyo, malalamiko ya mbunge huyo yalikatishwa na kelele za wabunge waliomtaka kupeleka hoja
hiyo kwenye vikao vya chama kwa kuwa hapo hapakuwa si mahali pake.
“Hayo malalamiko yako uyapeleke katika vikao vya chama chako vikashughulikiwe,” alisema Ezekiah Wenje (Nyamagana - Chadema) na kuungwa mkono na wabunge wengine.
Mbunge wa Nkenge, (CCM), Assumpta Mshama alisema rushwa iko njenje na katika kipindi hiki Bunge linaendelea, kwa kuwa kwenye jimbo lake kuna watu waliitwa na kupatiwa Sh10,000 kila mmoja hadharani.
“Watu wanaahidi kutengeneza vyoo, barabara wanatengeneza… Watu wako (watumishi wa Takukuru) wamekaa muda mrefu wamezoeleka. Kwa nini sasa hivi msiwabadilishe?” alihoji Mshama.
Sheria ya Gharama ya uchaguzi
Wabunge hao pia walilalamikia sheria ya Gharama za Uchaguzi kutoendana na hali halisi.
Mchungaji Peter Msigwa (Iringa Mjini - Chadema), Felix Mkosamali (Muhambwe - NCCR- Mageuzi) na Wenje, walisema kutokana na kushuka kwa thamani ya shilingi,  bidhaa na huduma zimepanda bei na kuifanya sheria hiyo kutokuwa na uhalisia katika hali ya sasa.
“Watu wataleta risiti kuwa wametumia Sh50 milioni kumbe ukienda katika uhalisia unakuta ametumia Sh200 milioni. Kama haitafanyiwa marekebisho kabla uchaguzi utekelezaji wake hautakuwa na uhalisia,” alisema Wenje.
Rushwa ya Mtandao
Mbunge wa Nkasi Kaskazini (CCM), Ally Keissy alisema baadhi ya wagombea wamekuwa wakitumia mitandao kugawa rushwa na kuihoji jinsi Takukuru itakavyowadhibiti.
Mbunge wa Simanjiro(CCM), Christopher Ole Sendeka, alisema Ikulu imewasafisha waliohusishwa na tuhuma za Akaunti ya Tegeta Escrow na kuhoji iwapo kitendo hicho hakitaathiri Takukuru na uchunguzi wake.

Akijibu hoja hizo, Dk Hoseah alisema taasisi yake haikurupuki katika kuwakamata watuhumiwa wa rushwa na imekuwa ikifanya uchunguzi wa kina kabla ya kuwakamata.
“Wale mnaotumia mitandao ya simu kutuma rushwa mtaumia vibaya katika uchaguzi huu. Ukituma tu rekodi inajionyesha labda sijui utumie lugha gani? Lakini ni rahisi sana kuwapata hawa wa mtandao kuliko wa guest (nyumba za kulala wageni),” alisema.
Kuhusu escrow alisema si kazi ya Takukuru kuwasafisha watuhumiwa, yenyewe inapeleka shauri kwenye mahakama ambayo ndiyo yenye mamlaka ya kuamua.
“Tunaendelea na uchunguzi na kwa wale walioko mahakamani wataendelea kujibu huko. Hatuna mpango wa kufuta kesi sisi tunafuata sheria inavyotuelekeza,” alisema. Kuhusu watendaji wa taasisi yake kukaa sehemu moja miaka mingi alisema kuanzia Januari hadi sasa wametumia Sh1 bilioni kuwahamisha.... “Huwezi kuhamisha mtumishi mmoja tu ni lazima uhamishe watatu na gharama ya kuhamisha mtumishi mmoja si chini ya Sh7 milioni. Hii inatosha sasa maana tukiendelea kuwahamisha tutakosa fedha za kufanya kazi.”
  Chanzo;Mwananchi
Toa maoni yako kwa habari hii kwa kuweka email yako hapa,na endelea kutufatilia zaidi Ukurasa wa habari

0 comments:

 
Supported by AMAGA Media services : | |
Copyright © 2015. UKURASA WA HABARI - All Rights Reserved
Templete Designed by Abdallah Magana
Proudly powered by Blogger